Thursday, October 6, 2011

Sarah Palin hatagombea Urais Marekani

Aliyekuwa gavana wa Alaska Sarah Palin ametangaza hatawania kiti cha Rais wa Marekani mwaka ujao.
Bi Palin amesema katika taarifa kuwa alifikia uamuzi huo baada ya kuzingatia mengi na kuwa yeye na mumewe wamejitolea katika masuala ya Mungu,familia na nchi yao.
Tangazo hilo la Palin mwenye umri wa miaka 47 limemaliza wasiwasi uliokuwepo kuhusu mipango yake.
Gavana wa zamani wa Massachusetts Mitt Romney na gavana wa Texas Rick Perry wanaongoza timu ya Marepublican kukabiliana na Rais Barack Obama katika kinyang'anyiro cha Ikulu ya White House mwaka ujao.
"Baada ya maombi mengi na kutafakari, nimeamua sitatafuta kuteuliwa kugombea kiti cha Rais wa Marekani" Bi Palin aliandika haya katika barua aliyowaandikia wafuasi wake.
"Kwangu, familia yangu ndio inachukuwa nafasi ya kwanza, mimi na Todd tumeweka familia yetu mbele kwanza kabla ya kuchukuwa uamuzi huu.
Lakini Palin amesema katika wiki zijazo atafanya mikakati ya kampeini kusaidia kumuondoa Rais wa sasa mamlakani, kumiliki bunge la Senate na bunge la Waakilishi.
Sarah Palin hakuonesha anamuunga nani mkono kati ya wagombea wa sasa wawili wanaotaka uteuzi wa chama ili wakabiliane na Obama.
Tangazo lake limetolewa siku moja baada ya gavana wa New Jersey Chris Christie kujiondoa katika kinyang'anyiro hicho.

No comments:

Post a Comment